Serikali imezitaka taasisi za lishe kushirikiana na sekta ya afya katika kutoa elimu kuhusu lishe kwa mama wajawazito, hatua ambayo inalenga kupunguza vifo vya mama na mtoto nchini.
Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, alitoa wito huo leo bungeni Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Neema Lugangira, aliyehoji juu ya jitihada za serikali katika kuhakikisha kila kituo cha afya nchini kinakuwa na wataalamu wa kutoa elimu ya lishe kwa mama wajawazito.
“Suala la lishe linahitaji ushirikiano mkubwa kati ya taasisi za lishe na sekta ya afya. Tunaendelea kuhamasisha na tunataka idadi ya akina mama wanaohudhuria kliniki ifikie asilimia 100 kutoka asilimia 92 iliyopo sasa, ili tuweze kushughulikia changamoto hii kikamilifu,” alisema Dkt. Mollel.
Kupitia mkakati huu, serikali inalenga kuongeza uelewa miongoni mwa wanawake wajawazito kuhusu umuhimu wa lishe bora na sahihi wakati wa ujauzito na baada ya kujifungua.
SomaZaidi;Mpango wa Afya Ngazi ya Jamii Pwani
Elimu hii itasaidia kupunguza hatari za kiafya kwa mama na mtoto, kama vile upungufu wa damu na matatizo mengine ya lishe yanayoweza kuepukika.
Kwa mujibu wa Dkt. Mollel, serikali inathamini umuhimu wa kutoa elimu sahihi na ya kina kwa wanawake wajawazito katika vituo vya afya ili kuhakikisha wanapata lishe bora inayowasaidia kuwa na afya njema wakati wa ujauzito na kuwezesha watoto kuzaliwa wakiwa na afya njema.
Hatua hii inaonesha azma ya serikali ya Tanzania katika kuboresha afya ya uzazi na mtoto kwa kuzingatia elimu ya lishe, ambayo ni msingi muhimu katika kujenga jamii yenye afya bora na maendeleo endelevu.